1
Awali naomba niwatake radhi kwa kuendelea kutumia neno ‘conductor’ mpaka sasa nimeshindwa kupata tafsiri yake kwa Kiswahili. Najua wengine wanamwita ‘mpimishaji’ na wengine’ mwongozaji’ au ‘mwimbishaji’. Naomba niendelee kutumia neno ‘conductor’ ili niwe huru kidogo.
Conductor ni kiongozi wa kundi la wanamuziki anayewakilisha uwajibikaji (responsibility) na mamlaka(authority). Tendo analofanya ni sanaa ya kuongoza na kuelekeza upigwaji/uimbwaji wa muziki kwa kutumia ishara zinazoonekana wazi (visible gestures). Kimsingi, wajibu wa conductor ni:
1. kuwaunganisha wanamuziki
2. Kuweka mwendo sawa (set the tempo)
3. Kuongoza maandalizi na mapigo
4. Kusikiliza kwa umakini (critical listening)
5. Kuunda/kutengeneza (shape) sauti za kundi linalopiga muziki.
Conuctor hupatikana katika bendi za muziki wa concert, orchestra, kwaya na makundi-unganishi ya muziki ( musical ensembles). Conductor kwa kawaida hushika aina ya fulani ya fimbo nyembamba nyeupe katika mkono mmoja kiitwacho ‘baton’ kwa ajili ya kuonesha mwendo na mapigo na mkono mwingine huutumia kwa vielelezo. Hata hivyo conductor anaweza kuongoza bila baton.



1. Kuwaunganisha wanamuziki:
Conductor anapaswa kujua aina ya muziki wanaopiga au kuimba. Anapaswa ajue pia aina ya ala za muziki zinazotumika. Nimetumia neno ala na sio vyombo vya muziki. Vyombo vya muziki (equipment) ni kama vile speaker, mixer.n.k. naongelea ala za muziki (musical instruments) kama vile ngoma, kinanda, n.k. Kwahiyo conductor anapaswa ajue jinsi atakavyowaunganisha wanamuziki (waimbaji na wapiga ala). Yeye ni kiongozi anayemtawala kila mmoja. Rafiki yangu Hekima Raymond anasisitiza kuwa ni lazima wanamuziki wamwangalie usoni hasa ishara atakazotoa kwa hisia za uzoni (facial expressions). Naam, conductor anaonyesha ishara kwa kutumia mwili wake hivyo wanamuziki ni budi wamwelewe kiongozi wao. Mfano, mpiga kinanda asianze wimbo kabla hajaruhusiwa na conductor. Conductor anaruhusu kuanza wimbo pale tu anapoona watu wake wako tayari (attentive) na sio huku mwingine anatafuta daftari, huyu mwingine anauma kucha z a vidole na mwingine ananong’ona na mwenzake. Wote wawe katika u tayari (attention).

Kazi kubwa ya conductor hufanyika wakati wa mazoezi. Kwenye mazoezi ndipo anapowazoeza kuhusu ufundi wa wimbo ( technical aspect) na hisia zinazoonekana katika wimbo. Yeye ndiye anapaswa kufanya kikundi kipige/kuimba vile anavyotaka. Anabuni (imagine) jinsi wimbo unavyotakiwa kusikika na hivyo kutumia muda wa mazoezi kufika anakotarajia, yaani jinsi alivyobuni kichwani kwake ndivyo iwe. Hapa nizungumzie mtazamo wa sanaa. Katika sanaa huwa tunaanza mwisho na kuja mwanzo. Mfano msanii mchoraji, kabla hajaanza kuchora ni lazima kwanza awe na picha anayotaka kuchora katika mawazo yake. Akishakuwa na hiyo picha kichwani ndipo anapoweza kuchora kuelekea au kufuatana na picha iliyo kichwani kwake. Kwahiyo tunaweza kusema kuwa picha ilishakuwepo kichwani kwake kabla haichora tukaiona. Karibu na nyumbani kwangu kuna kijana alifungua kiosk akamwita mchoraji achore picha ya Bob Marley. Mchoraji akafanya kazi yake, alipomaliza tukaona sio sura ya Bob Marley ila ya mwanamuziki wa Marekani Buster Rhyme! Inaonesha kuwa mchoraji hakuwa nafahamu vizuri kichwani kwake sura ya Bob Marley na kosa dogo likapelekea picha kuhamia kwa Buster Rhyme. Na conductor pia ni vizuri awe na picha ya muziki unavyopaswa usikike, wakati anausoma iwe ausikie kichwani kwake na afanyie kazi kuelekea huko, hapo anaweza kufanya mabadiliko katika wimbo hasa mwendo na hisia (tempo & dynamics)iwapo mtunzi hakuziandika au hazitoshelezi picha aliyonayo conductor wetu. Conductor asitegemee kufanya maajabu siku ya kuimba (performance) ikiwa hakuwazoeza kabla, kumbuka – ng’ombe hanenepi siku ya mnada! Tukiosikia na kuona jinsi walivyoimba na kupiga wimbo ndipo tunajua mazoezi yao yalivyokuwa, hii ni kanuni ya garbage in-garbage out!

2. Kuweka mwendo sawa:
Nimeelezea hapo juu kuwa conductor anaweza kufanya mabadiliko katika wimbo kuhusu mwendo. Ila ni vizuri kwanza ausome wimbo na kuelewa hisia za mtunzi kabla hajaweka za kwake. Hisia atakazoongeza zisiharibu wimbo.

3. Kuongoza maandalizi:
Conductor anasimamia vilivyo mazoezi ili, kama nilivyosema awali, siku ya tukio kitoke kile alichotarajia na si vinginevyo.
 
4. Kusikiliza kwa umakini:
Conductor mzuri ni Yule mwenye ‘sikio la muziki’. Katika mazoezi atahakikisha waimbaji na wapiga ala wote wanaimba na kupiga noti katika kiwango (pitch) na mwendo sahihi. Wakiwa jukwaani anaendelea na kazi yake ya kusikiliza na pale penye tofauti ni kazi yake kumjulisha mhusika., iwapo ni alto wanakwenda off-pitch awape ishara ili warekebishe. Sio vizuri aendelee kufurahia midundo wakati pitch inaharibika!

5. Kutengeneza sauti:
Hii ni ni kazi yake kuleta uwiano kati ya ala na sauti za waimbaji. Kama si mtaalamu wa kunoa sauti (vocal trainer) apawepo na mtaalam huyo halafu conductor atashughulikia hisia za wimbo.

Kabla sijaendelea mbele kuelezea sifa na wajibu wa conductor nimeona niongelee hapa mazingira ya kwaya zetu. Kilichonisukuma kufanya hivi ni maoni ya wadau wale walioandika kuwa hapa kwetu basi hatuna conductors wa kweli. Mazingira yetu ni tofauti. Nitajadili. Mazingira yetu ya kwaya zetu ni magumu mtu kuwa mkamilifu kwa 100% ya conductor mzuri , hata kwa 75%! Kwa sababu
1.      Kwaya ndizo zenye jukumu la kuongoza waumini katika uimbaji kwenye Misa na Ibada mbali mbali. Misa moja inaweza kuwa na uhitaji wa nyimbo 15 (makisio ya chini) na zote zinaongozwa na kwaya. Muda wa kupitia nyimbo (pieces) nzuri za classical au zenye ufundi mkubwa hakuna. Wanaoziimba wanajua wenyewe jinsi jitihada ya ziada ilivyofanyika. Madhehebu mengine kwaya si kiongozi wa nyimbo. waumini wote wanaimba kwqa kutajiwa namba ya wimbo, organist anaanzisha kisha kanisa zima wanafuata huo wimbo. kwaya ina sehemu yake inaitwa na kuimba ujumbe wao. mara nyingi ni wakati wa sadaka na meza ya Bwana (Komunyo). Hapo kwaya inaweza kujianda vizuri zaidi kwa vile wana nyimbo 2 tu kwa ibada nzima.
 
2.      Kwaya zinaweka nyimbo mpya kila Dominika. Katika Misa kwaya haiwezi kukwepa Wimbo wa mwanzo, Katikati, Shangilio na Wimbo wa Komunyo. Hizi ni kama mpya kwa sababu kuna mwaka A, B na C (bila kutaja sherehe katika kalenda ya kanisa) zinakumbushwa kwa namna ya kufundishwa tena na pengine zinatungwa mpya. Muda unakuwa mdogo kupitia mambo ya kiufundi katika nyimbo zetu. Ndio maana kuna neno "ku-brush". hata muda wa kunoa sauti (vocal training) hatuna.
 
3.      Wingi wa nyimbo, tuseme 20, katika Misa unaweza kumfanya conductor asahau Alama ya wakati (Time signature) katika baadhi ya nyimbo, akajikuta 4 4 anaongoza kama 2 4, 3 8 anaongoza kama 6 8. Nyimbo ni nyingi kukumbuka kila kipengee cha dynamic na expression. Kwenye tamasha ni raihisi kwa sababu huwa hazizidi nyimbo tatu kwa kila kwaya.
 
4.      Elimu ya muziki. Narudi pale pale, mbali ya kuwa baadhi ya conductors hawana elimu sahihi ya muziki lakini hata wapiga ala pia mfano wapiga ngoma. Kila mara nasikia upigaji wa ngoma wa 3 4 hautofautishwi na 6 8. Ngoma ndio inayotupatia rhythm na bahati mbaya wapigaji wengi wa siku hizi hawajui pigo la mkazo (accent beat) wanashabikia kuchanganya zile ngoma ndoigo kwa muda mrefu bila kupiga ngoma yenye pigo kubwa. Natamani siku moja nifanye workshop na wapiga ngoma! Mpiga ngoma asiyejua Alama ya wakati atatofautishaje upigaji kati ya wimbo na wimbo?
 
5.      Shughuli za maisha. Wanakwaya si watu wanaoimba kama professionals ( kukidhi mahitaji ya maisha kwa uimbaji tu) bali ni watu wanaojishughulisha na ajira, kilimo, biashara au masomo. Wanakuja kuimba mara tu baada ya kumaliza shughuli hizo -mazoezi yanachelewa. Anaweza kuwepo katika mazoezi kimwili lakini kifikra hayupolabda kuna tatizo kazini au nyumbai - utafundisha lakini hashiki kiurahisi. Siku unayomtegemea yeye amebanwa na kazi inayomletea mkate wake wa kila siku - performance itashuka kiwango au itaharibika. katika baadhi ya parokia nilizotembelea nimekuta wanamaliza mazoezi saa 12:30 jioni. Walianza saa ngapi? 11:45! kwa muda huo utapitia nyimbo ngapi kwa ufasaha zaidi?
 
6.      Mazoea: Kila jumapili mtu anaimba, anazoea na kuona kuimba ni kitu cha kawaida kiasi kwamba huhitaji mazoezi, tofauti na tamasha ambapo halifanyiki kila jumapili na hivyo watu kujiandaa sana kwa tukio hilo. Ndio maana ninapenda sana parokia zinazofanya tamasha walau mara moja kwa mwaka, inasaidia kuondoka katika uimbaji, uongozaji na upigaji wa nyimbo kwa mazoea. 
Kwa ujumla niseme tu, tuwatumie waliopo na tuwape moyo katika kujitolea kwao. Tuwaelekeze kwa unyenyekevu kule wanakopaswa kwenda iwe ni elimu au ujuzi zaidi wa muziki.


SIFA ZA CONDUCTOR: 
1. Elimu ya muziki:
Nimeweka elimu ya muziki kama sifa ya kwanza kwa sababu kwa mtazamo wangu, bila elimu kuna mambo yatavurugika. Elimu ya muziki nadharia, vitendo na utunzi ni silaha nzuri kwake. Nyimbo zinaandikwa, kwahiyo zinahitaji elimu fulani kuzisoma na kuzielewa kilichomaanishwa. Maelekezo mengi anayotoa conductor kama vile Alama ya Wakati (Time Signature) , maelekezo ya upigaji (performance expressions) ni mambo yanayohitaji elimu ya muziki. Nimeona baadhi ya conductors hawatofautishi kati ya 2 4 na 4 4, au kati ya 3 8 na 6 8. Elimu ya muziki kwa kiwango cha wastani huku kwetu itamfanya conductor awajibike vizuri. Katika nchi zilizoendelea, conductor wa orchestra anakuwa na degree ya muziki, kwao hiyo nafasi ina heshima sana.
 
2. Ufahamu wa ala mojawapo ya muziki:
Conductor anayefahamu kupiga walau ala mojawapo ya muziki anakuwa na faida ya ziada. Ala itamsaidia kuwa na ‘sikio la muziki’ na vile vile aweze kumwelekeza mpigaji wa ala hiyo nini cha kufanya katika wimbo. Akijua ala moja itasaidia kumpa picha ya mpigaji kihisia na mtazamo kuhusu wimbo.

3. Msomaji mzuri wa muziki papo kwa hapo(sight-reader):
Usomaji wa namna hii kwanza hutokana na elimu na pili, uzoefu. Akishapata elimu conductor ajizoeze kusoma nyimbo nyingi mara kwa mara ili akumbane na changamoto mbali mbali za nyimbo na vionjo tofauti kutoka kwa watunzi tofauti. Mazoezi ni jambo la msingi. Huwa nawaambia wanafunzi wangu kuwa hakuna miujiza ya mtu kuweza kusoma muziki haraka, vizuri na kwa usahihi au kupiga kinanda vizuri isipokuwa kwa mazoezi tu – practice maketh perfect!
 
4. Mdadisi na mtafiti:
Udadisi humfanya mtu ajielimishe zaidi. Udadisi ni kiu ya kutaka kujua jambo fulanikwa undani zaidi. Mtu ambae si mdadisi anaweza kubaki hapo alipo kwa miaka nenda rudi, huyu hatufai katika kuinua kikundi kimuziki kutoka ngazi moja kwenda nyingine. Conductor awe mdadisi wa kuuliza wengine wanaojua, kuhudhuria matamasha, kusikiliza nyimbo za wengine waliomzidi kiwango , kusoma vitabu na siku hizi mtandao una kila kitu, ajielimishe zaidi, asibweteke hata akisifiwa namna gani. Tena aangalie anasifiwa na nani. Mtu wa kawaida ana vigezo vya kukusifu na mtaalamu wa muziki atakusifu pia kwa vigezo, sasa inategemea unabeba zaidi sifa zipi. Ningeshauri ubebe sifa za mtaalamu wa muziki, ziwe mbaya au nzuri. Mfano. Mtu akipiga kinda kwa ‘single touch’ kutoka mwanzo wa kinanda mpaka mwisho mara moja prrrrrrrrrrrrrrrr(nadhani naeleweka, inasikika sana hii kwenye sebene zetu siku hizi) watu wa kawaida watashangilia na kusema kuwa jamaa anajua sana kupiga kinanda, lakini mtaalamu wa muziki hataona ufundi wowote hapo kwani hata panya akidondokea hizo keyboard buttons akakimbia juu yake mara moja bila shaka kinanda kitatoa mlio huo huo prrrrrrrrrrrrrrrrrr, sasa hapo tutasema kuwa panya anajua kupiga kinanda? Mtaalamu ataangalia ule uchambuzi wa noti na noti ili kuleta muziki mzuri unaowiana. Sifa zisikufanye ukose udadisi. 

5. Anayeweza kutawala hisia zake:
Kutawala hisia zote nzuri na mbaya. Hisia mbaya ni kama vile hasira, huzuni, kukata tama. Hizi hazifai hasa siku ya onesho (performance). Wanamuziki wanamsoma conductor usoni wanamwelewa hata akikasirika lakini hisia hizi (mbaya)zinapokuwa wazi mno mpaka hadhira (audience) yote ikafahamu inakuwa haipendezi. Conductors wengine hutoa maneno makali na shutuma wanapofanya onesho iwapo kuna kitu hakiendi sawa kwa wanamuziki wake. Hisia nzuri ni kama vile furaha. Conductor asifurahi kupita kiwango, akatekwa na midundo au mashangilio ya watu na kusahau kufanya baadhi ya mambo ambayo waliyafanyia kazi katika mazoezi, mfano kupunguza sauti (piano, pianissimo) yeye akapita tu sehemu hiyo kwa kujawa na furaha na shangwe ya siku hiyo.
 
6. Mtu wa watu:
Ninaposema mtu wa watu nina maana kuwa ni mtu mwenye mahusiano mazuri na wengine, mtu rahisi kushaurika, kusikiliza wengine na kujenga nidhamu ya kikundi. Kitabia awe mtu mwenye utaratibu katika mambo yake. Kuna mwingine leo anaanza wimbo huu, kesho anakuja na mwingine wakati ule wa mwanzo hajaumaliza, hafai. Awe mtu wa kuwajenga kisaikolojia wanamuziki wake. Kwenye kukata tama awape moyo, kwenye makosa asahihishe kwa upendo na uvumilivu. Asilewe sifa na asiwape sifa isiyostahili watu wake. Ajiweke katika namna ambayo watu wake wanamwelewa.

.....itaendelea

Shukrani za pekee kwa Mwl. Richard Mloka

Na chanzo cha habari http://www.swahilimusicnotes.com/page/nafasi-na-kazi-ya-conductor-by-richard-mloka


Chapisha Maoni

Unknown alisema ... 14 Novemba 2016, 16:05

Kwa kiswahili anaitwa Mtiribu.

 
Top