0
Bikira Maria kupalizwa mbinguni. Kanisa Katoliki linajivunia kwa imani hiyo kwani linaamini na kusadiki tendo hili la Mungu kumpaliza mbinguni mwanamke Pekee duniani aliyeshiriki ukombozi wa mwanadamu.
Ijapo Kanisa linakumbwa na changamoto kutoka kwa watu wanaohoji na kukataa tendo hili la imani, msimamo wa mafundisho ya Kanisa unabaki palepale kwani ni kweli Bikira Maria amepalizwa mbinguni.
Fundisho la Kupalizwa Bikira Maria mbinguni mwili na roho, linatakiwa limakinike kwanza kwa lugha ya kiimani.
Ni hivi, Kanisa Katoliki lina chemichemi moja ya kimungu ya ufunuo lakini chemichemi hiyo hutiririka kwa mikondo miwili iliyo na thamani sawa, yaani Maandiko Matakatifu na Mapokeo Matakatifu.
Kwa kushindilia maelezo yangu, katika makala hii, nitawavusheni hata nje ya mikondo hiyo rasmi. Nia yangu ni kutoa maelezo ya kuwashibisheni ninyi wasomaji wapendwa.
Kwa faida yetu sote, aheri leo tuanze na maelezo ya Mapokeo Matakatifu na baadaye tuingie kwenye Maandiko Matakatifu, madhali mikondo yote miwili itathibitisha fundisho hili hili moja.
Zaidi ya hilo, natumaini kwa mtindo huu wa kulitazama fundisho hili, nitathibitisha pia kwamba imani ya Kikristo haikuanza na maandishi isipokuwa na mambo yaliyoshuhudiwa au kuaminiwa na wafuasi wa mwanzo na kisha wao kutuandikia sisi.
Hivi Maandiko Matakatifu ni mtoto wa Mapokeo Matakatifu, na si kinyume chake kama wengine wanavyotaka kutuvuruga wenzao kwa hoja na madai batili. Kuthibitisha hili, Maandiko Matakatifu yenyewe yanakiri kwamba si yote yaliyofanyika wakati wa Yesu yaliandikwa. Kwa kifupi, ni kwamba yaliyoandikwa ni baadhi tu ya mengi yaliyoshuhudiwa au kuaminiwa (rej. Yn 20:30-31 na 21:25). Tusome
sehemu hizo na tuzitafakari bila jazba.
Kumbe, tumeandikiwa hivi: “Basi, kuna ishara nyingine nyingi alizozifanya Yesu mbele ya wanafunzi wake, zisizoandikwa katika kitabu hiki (yaani Biblia au Injili). Lakini hizi zimeandikwa, ili mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa  Mungu na kwa kuamini muwe na uzima kwa jina lake. Kuna na mambo mengine mengi aliyoyafanya Yesu ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa  vile vitabu vitakayoandikwa”.

Mapokeo Matakatifu
Basi, tuanze na mkondo wa Mapokeo Matakatifu. Tukianza na Mapokeo Matakatifu, ni hivi tangu zamani  makanisa ya Mashariki (ya  Kiorthodoksi) na Magharibi (Kanisa Katoliki) yalikuwa yakisherehekea sikukuu hiyo kwa namna moja au nyingine. Ndiyo maana wakati wa karne ya saba, yaani enzi za Baba Mtakatifu Sergio, kulikuwa na sherehe ya “Kulala au Kusinzia kwa Bikira Maria (Dormitio). Baadaye mambo yalihamishiwa tarehe 15 Agosti.
Kumbe, ushahidi wetu wa kwanza ni kutoka kwenye Mapokeo. Mapokeo ni nini? Ni mambo yale yanayohusu imani ya kikristo ambayo hayakuandikiwa. Na tukumbuke hapo mwanzo, Ukristo ulienezwa kwa masimulizi ya mdomo tu kwani Yesu hakuwa na kitabu na wala hakuwaagiza watu waandike habari za maneno na matendo yake.
Vitabu vya kwanza ni barua mbili kwa Wathesalonike, vitabu vilivyoandikwa na Paulo kwa hiari yake mwenyewe, yaani pasipo shinikizo la mtu yeyote. Mitume wote walitumaini masimulizi ya mdomo kwani ukiachilia mbali Agano la Kale hawakuwa na kitabu chochote kilichohusu habari za Yesu.
Barua hizo ziliandikwa mwaka 50 au 51. Injili ya kwanza ilikuja mwaka 70 BC yaani miaka kama 37 baada ya Yesu kufa, kufufuka na kupaa mbinguni. Hiyo ilikuwa Injili ya Marko, zikafuatia Injili za Mathayo na Luka kati ya mwaka 80 na 85 na mwishowe Injili ya Yohane kati ya mwaka 90 na 100. Kushuhudia kwamba mitume na wafuasi wa Kristo hapo kwanza walitumaini mafundisho ya mdomo yaani Mapokea na wakaandika mambo hayo katika miaka ya baadaye soma 1 Kor 11:23, 15:1-3, Gal 1:9.12, Flp 4:9, Kol 1:12, 1 The 1:6 na 2 The 3:6.
Ndipo, kwa kadiri ya Mapokeo ya Wakristo wa karne ya mwanzo, Bikira Maria alifariki na kuzikwa huko Yerusalemu, karibu na maeneo ya bustani ya Gethsamane, ambako kaburi lake lipo mpaka leo hii. Tunafahamu Bikira Maria aliishi duniani na watu walimfahamu vyema katika Kanisa la mwanzo.
Bikira hakuishi peke yake bali aliishi na watu wengine wengi tu. Yaliyompata watu hao waliyaona, kuyasikia na hata kuyashuhudia. Basi jinsi alivyoyamaliza maisha yake ya kidunia watu hao wana habari nayo kwani walikuwepo pamoja naye na si wewe na mimi tunaobisha leo hii.
Bikira Maria aliyamaliza maisha yake kwa kulala au kuzinzia ambako Mungu alimbadilishia mwili wake wa kibailojia kwenda kwenye mwili wa kiroho, mwili ambao kila mmoja atauhitaji ikiwa anataka kuishi milele. Hakuna mtu atakayeweza kuishi milele na mwili huu wa kibailojia. Ni lazima awe na mwili wa kiroho. Tulio wengi tutaupata mwili wa namna hiyo siku ile ya ufufuko wa wafu.
Basi, kutokana na maelezo ya watu walioishi na Bikira Maria na kushuhudia jinsi alivyomaliza maisha yake ya kidunia kwa mtindo wa ajabu Kanisa linatueleza kwamba sikukuu ya kupalizwa Bikira Maria mbinguni mwili na roho ilianza kuadhimishwa tangu karne ya sita ambapo ilikuwa ikiitwa kulala usingizi au kusinzia kwa Maria.
Mapokeo pia yanatupatia sababu kadhaa kuthibitisha kuwa Bikira Maria alipalizwa mbinugni mwili na roho.
Kimuhtasari, sababu za kupalizwa mbinguni ni kadhaa lakini tuziweke daima mbele yetu sababu nne: kukingiwa dhambi ya asili, umama wake wa Mungu (Yesu Kristo), ubikira wake na kushiriki kwake kikamilifu katika kazi ya ukombozi pamoja na mwanawe. Usihangaike. Nazifafanua hoja sasa hivi.
Kwanza, Bikira Maria hakuwa na dhambi ya asili, kama tulivyoeleza hapo juu, hivyo hakuwa na doa. Kwa hali hiyo, hakustahili kufa na kuoza jambo ambalo ni adhabu iliyotokana na dhambi ya asili, adhabu ambayo wewe na mimi hatukujaliwa kuiepuka. Kumbe, Bikira Maria alizaliwa akiwa na uzima wa neema ya utakaso. Ndipo, mwili wake haukuharibika. Kwa hiyo, alistahili achukuliwe mbinguni mwili na roho.
Kumbe, mambo yalianzia kwenye ukweli kwamba tangu milele Mungu alikusudia kumtakatifuza na kumtukuza Bikira Maria kwa namna ya ajabu. Alimkingia dhambi ya asili ili Mwana wa Mungu, aliye mtakatifu (rej. Lk 1:35), afikie patakatifu. Kama ajapo mfalme wa kidunia tu, watu huangaika kukiandaa chumba atakachofikia, haikuwa zaidi sana kwa ujio wa Masiya, Mtakatifu, Mwana wa Mungu?
Mbona Rais anapotembelea mahali fulani watu huchonga barabara, kupaka rangi nyumba na kuandaa kitanda kwa shuka mpya? Sasa Mungu asiandaliwe mahali anapofikia? Basi, ilimpendeza Mungu kumwandaa Maria kabla Yesu hajatungwa mimba. Ndipo “akampiga deki sana” ndiyo huko kumkingia dhambi ya asili inayochafua maelekeo na tabia za watoto wote wa Adamu na Eva.

TUNAKAZIA ukweli wa Bikira Maria kukingiwa dhambi kabla ya kumzaa mtoto wake mtakatifu. Mtu hawezi kumpokea mgeni halafu akaanza kukisafisha chumba chake wakati mgeni mwenyewe amekwisha karibishwa ndani.
Mafundisho haya yamefumbuliwa na Mungu na yamefundishwa na walimu wa Kanisa tangu mwanzo wa Kanisa. Papa Pio IX, kama mwalimu na mchungaji mkuu wa Kanisa lote, kwa msaada wa Roho Mtakatifu alitangaza mafundisho hayo tarehe 8 Desemba 1854. Kwa maneno haya kuwa Bikira Maria amekingiwa dhambi ya asili yaani ile dhambi tuliyoirithi sisi kutokana na kosa la kwanza walilolifanya wazee wetu Adamu na Eva.
Bikira Maria alikingiwa dhambi ya asili kusudi awe safi, mtakatifu, asiye na doa lolote toka mwanzo wa uhai wake ili kutuletea Mkombozi yaani Bwana wetu Yesu Kristo.
Kuzaliwa kwa Bikira Maria ni kama pambazuko la alfajiri yaani ujio wake ndio dalili kwamba Mkombozi mwenyewe hawezi kukawia kuonekana. Kanisa limetunga wimbo huu, “Kuzaliwa kwako, ee Bikira Maria, Mama wa Mungu kumeleta habari ya furaha kwa watu wote wa dunia, kwa sababu ndiwe uliyemzaa Jua la Haki, yaani Yesu Kristo Mungu wetu.”
Pamoja na kusema haya yote, hatuna budi kuongeza kwamba kutokana na matokeo ya Mama Bikira Maria kwa watu mbalimbali hapa duniani mfano kule Lourdes na Fatima tunapata ushahidi wa ziada kwamba Bikira alikingiwa dhambi ya asili na pia kwamba alipalizwa mbinguni mwili na roho. Hayo tunayajua kutokana na mwonekano wake pamoja na kauli zake mwenyewe kwa hao aliowatokea.
Pili, Bikira Maria ni Mama wa Mungu. Mwili wake ulimchukua mimba Mwokozi Yesu Kristo. Ndipo basi, kutokana na uhusiano wa karibu sana uliokuwepo kati ya Bikira Maria na Yesu, Yesu asingelisita kuutukuza mwili wa mama yake uliomchukua mimba.
Tatu, ni kwamba Bikira Maria alibaki Bikira daima. Ubikira wake haukudhurika. Ndipo basi, ilistahiki kabisa mwili wake ambao haukudhurika usioze wala kuharibika.
Hatimaye, sababu ya mwisho ni kwamba Bikira Maria, alishiriki kazi ya ukombozi, yaani alifaulu kuambatana sana na mwanawe. Aliambatana naye katika furaha na katika uchungu. Akiwa duniani, Mama Bikira Maria ameshiriki kazi ya ukombozi ulioletwa na mwanaye Yesu Kristo kwa kufanya yafuatayo: kukubali kumzaa Mkombozi Yesu Kristo, kumtoa Yesu hekaluni, kuvumilia taabu za Misri, kumtafuta Yesu aliyebakia hekaluni, kumsihi Yesu awasaidie watu  kwenye harusi ya Kana, kushuhudia njia ya mateso ya mwanawe, kushuhudia kifo cha mwanawe msalabani  na hatimaye kushuhudia mazishi yake.
Hivyo, Bikira Maria ameshiriki katika kazi ya ukombozi ya mwanawe kwa kukubali kwa hiari yake kuvumilia mambo magumu mengi kwa kuwa Mama wa Mkombozi (rej Lk 2:35). Kisha ameshiriki katika kazi ya ukombozi pale alipomtolea Mungu Baba mateso yake pamoja na mateso ya Yesu ili dhambi za watu ziondolewe.
Alipata taabu tangu utotoni mwa Yesu kwa kulazimika kwenda naye ukimbizini. Wakati wa Yesu kuutangaza ufalme wa Mungu kulikuwa na matukio chungu mzima ambayo Bikira Maria, kama mama aliionja vilivyo. Hata pale msalabani, Bikira Maria alikuwepo chini ya msalaba akiugulia maumivu ya mwanawe mpenzi ambaye watu walimsulubisha bila huruma na walikuwa wakimkejeli kama gaidi au mhalifu.
Ndiyo maana ya unabii wa mzee Simeoni ambaye alisema kwamba upanga wa mateso ungepenya roho yake pia. Hivyo, uhusiano huu wa karibu ulibidi usiishie hapa duniani bali uendelezwe hata mbinguni. Basi Bikira Maria amepata tuzo la kushirikiana na Yesu katika taabu na raha. Ni ukweli wa kudumu kwamba mtu yeyote anayeshiriki katika mapinduzi yoyote yenye mafanikio lazima atuzwe cheo cha maana.
Acha tuendelee. Ndugu yangu, kama tulivyosema hapo juu, Mapokeo yametujuza kwamba Bikira Maria alikufa ili abadilishe mwili huu na kupata mwili wa utukufu wenye uwezo wa kuishi milele. Ndiyo kisa basi, imani yetu inashuhudia uwepo wa Bikira Maria mbinguni mwili na roho. Basi pamoja na Yesu Kristo, katika hali ya mbinguni, mtu wa pili mwenye mwili na roho ni Bikira Maria.
Maandiko Matakatifu

Sasa tuhamie kwenye Maandiko Matakatifu. Wala si siri, ndugu zangu kwamba Wakatoliki hukabiliwa kila kukicha na madai ya watu wasiompenda Bikira Maria dhidi ya fundisho la kupalizwa kwake mbinguni mwili na roho. Katika madai yao, watu wa namna hiyo hudai eti hakuna ushahidi wowote wa kimaandiko wa kuonesha kuwa Bikira Maria alipalizwa mbinguni mwili na roho. Yaani hukana yote wakisema kwamba hata kwenye Biblia hakuna dokezo lolote. Ndipo kwa ujumla watu hao huikana haja ya kuliamini fundisho hilo.
Ndugu zangu msidanganyike, kimaandiko, kuna ushahidi tosha wa kuonesha kuwa Bikira Maria alipalizwa mbinguni mwili na roho. Madokezo ya nguvu kwenye Biblia huanzia kwenye Yn 20:30-31 na 21:24-24 hadi kwenye Ufu 12:1-17.
Kisha kuna ushahidi wa kimapokeo kutokana na imani ya kale kabisa iliyochanua kwenye tangazo rasmi la tarehe 8 Desemba, 1854 na sambamba na ushahidi huo kuna mwanga katika kitabu kilicho nje ya chemichemi za ufunuo, ndiyo kitabu cha ‘apokrifa’ kiitwacho Kupalizwa Bikira Maria Mbinguni.
Habari za kitabu hiki zikichujwa sana, ukweli wa kiini hubaki kuwa Mungu alimpaliza Bikira Maria mbinguni mwili na roho kama zawadi ya nafasi yake ya kuwa mama wa Yesu Kristo. Basi kwa ushahidi uliopo ipo haja ya kuliamini fundisho hilo kwani ni fundisho la ufunuo wa kweli.
Sisi sote tunajua kwamba swali juu ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni mwili na roho ni moja ya maswali maarufu sana wanayobandikwa Wakatoliki. Huulizwa mara kwa mara na watu mbalimbali na kujibiwa na wataalamu mbalimbali tena kwa mitindo mbalimbali.
Maandiko Matakatifu: Tukienda kwenye Maandiko matakatifu, tunasoma katika Ufu 12:1-17 habari za mwanamke na joka. Imeandikwa, “Ishara kubwa ilionekana mbinguni. Mwanamke aliyevikwa jua na mwezi chini ya miguu yake na juu ya kichwa chake taji la nyota kumi na mbili.”
Kwa hakika, mwanamke anayeongelewa hapa kinabii si mwingine isipokuwa ni Mama Bikira Maria ambaye baada ya kufika mbinguni amefanyiwa mambo makuu mno. Kitabu cha Ufunuo wa Yohane ni kitabu cha unabii na unabii huongelea mambo kwa mtindo usio wa moja kwa moja na hivyo hutakiwa kueleweka kwa jicho la imani na unyenyekevu wa moyo. Mtu akitanguliza ubishi hawezi kuuelewa unabii.


  
Na Titus Amigu 
Padri wa Jimbo katoliki Lindi.



Chapisha Maoni

 
Top