0
Monika mwaka 331 huko Tagaste (Algeria). Tangu utoto wake alifundishwa kumtumikia Mungu na kujietenga na dhambi. Monika alizoea kwenda kusali peke yake kanisani, alikuwa akiwapenda maskini na aliwagawia chakula chake. Alipokua wazazi wake wakamwoza kwa kijana mmoja jina lake Patriki, naye ambaye alikuwa mtu wa ukoo bora, lakini hakuwa mkristu na mwepesi wa kukasirika. Monika alistahimili kwa upole alipogombezwa na mumewe. Alizaa watoto watatu na mmoja wao ndiye Augustino, Mwalimu wa Kanisa. Monika aliwafundisha kumpenda bwana wetu Yesu na kulitaja jina lake kwa heshima. Hata mume wake Patriki naye akaongoka akawa mkristu kwa sababu ya mwenendo safi wa Monika.

Augustino mwanawe alienda kukaa Kartago (Tunisia) ili asome shule, akaendelea katika maarifa yote, lakini alizidi kufanya uashereti na mambo yote yasiyofaa. Alimsikitisha sana mama yake. Monika alimwendea askofu mmoja wa huko akamuulizia. Itakuwaje na mwanangu? Naye askofu akamjibu “Usiogope mama, mtoto huyu wa machozi mengi hivi hawezi kuoptea”. Kweli Monika hakumwomba Mungu bure, maana Augustino aliongoka, akabatizwa na Mt. Ambrosi (taz 7 Desemba), akawa mwalimu shujaa wa mafundisho ya kanisa katoliki.
Monika alipojiona karibu kufa, aliwaambia wanawe: “Mnizike mpendavyo ila nawambeni kitu kimoja: Mnikumbuke kwenye altarehe ya Bwana”. Akafa huko Ostia (Italia) mwaka 387.
Sala ya Mama Mkristo kwa Maombezi ya Mt. Monika
Sala:
Mt. Monika, mwanamke na mama mwenye kuteseka, unajua machozi yangu, mahangaiko na uchungu wangu. Wakati fulani uliteseka kama mimi; naomba unionee huruma kwa mateso niliyonayo, Uniombee. Kutoka kwa Roho Mtakatifu ulipokea zawadi ya ufahamu na busara nguvu na sala. Uniombee ili nami nijaliwe zawadi zilezile. Kwa kuwa ulikuwa mpatanishi, daima uwaombee mume na watoto wangu na usali kwa ajili ya amani ya nyumba yetu.
Kwa maombezi yako uliwaokoa mumeo na mwanao. Utuombee neema ya Mungu ili tuwe na imani katika nyumba yetu. Kutokana na kuhudhuria Misa kila siku uliweza kupata nguvu na faraja; basi utuombee nasi nguvu na faraja katika maisha yetu daima. Utuombee kwa ajili ya mahitaji yetu muhimu ya kidunia; kusudi tuweze kufanya kazi na kuwa na amani katika familia yetu. Uwakumbuke watoto wangu, ili daima wajue pendo la kweli na hivyo wamtumikie Mungu kwa mapendo safi. Uniombee, ili niwe mama mwema kwao, na mwisho wa maisha haya, mimi pamoja na mume wangu, watoto wangu na wapendwa wangu wote tuweze kufika kwa Mungu, huko ambako wewe upo pamoja na mume wako na watoto wako wote. Kwa njia ya Kristo, Bwana wetu. Amina.
Mt. Monika, Mlinzi wa akina mama Wakristo. Utuombee.

Chapisha Maoni

 
Top