0
Je, ni kweli Kanisa Katoliki lina wadhifa wa “ukuu wa kanisa nchini”? Sheria ya kanisa {Can. 381(1)} inasema kila jimbo linaendeshwa na askofu wake. Hivyo Kardinali Pengo na uchungaji wake ni kwa Jimbo la Dar es Salaam bila kuvuka mipaka yake iliyozungukwa na majimbo ya Morogoro, Zanzibar na Lindi.
Kinachoitwa ukuu wa kanisa nchini, hakimo katika Sheria za kanisa (Canon Laws). Ukardinali unapodhaniwa ndiyo “ukuu” huo, basi ni ishara kuwa Kanisa Katoliki limesheheni masuala ambayo hufikia kutamkwa au kujadiliwa bila utafiti likiwemo hili la ukardinali.
Historia ya ukardinali inaambatana na Papa kuwa kiongozi wa kanisa duniani. Lakini Papa pia ni askofu wa jimbo la Roma. Hivyo anahitaji wasaidizi mbalimbali.
Neno Kardinali linatokana na neno la Kilatini cardo ambalo kwa Kiswahili ni “bawaba” yaani chuma kinachoushikilia mlango ukutani kwa kupigiliwa misumari. Mlango huo asili yake ni mti uliokatwa, ukachongwa na kutundikwa ukutani kwa bawaba.
Uhamisho wa watumishi wa kanisa kwenda jimbo jingine, ulifananishwa na ule mlango kuhamishiwa ukutani kwa kushikiliwa na bawaba (cardo). Hivyo zamani waliohamia jimbo lolote waliitwa “Cardinal” neno tunaloliita “Kardinali” au “Kardinali”.
Neno “meseji” linatamkwa hata na mtoto na tunaelewa. Lakini inasisitizwa kutamka neno “ujumbe”. Neno “Teolojia” limetamadunishwa na kuwa “tauhidi” au “taali-Mungu”. Huwa nawaza, kwa utamadunishaji huu sitoshangaa tukiambiwa tutumie neno “ubawaba” badala ya “ukardinali” ili iwe “Bawaba Polycarp Pengo” badala ya “Kardinali Polycarp Pengo”.
Ilipofika karne ya 9 haki ya kutambulika kama “Kardinali” ilibaki kwa baadhi ya waliohamishiwa jimbo moja tu la Roma au jimbo la Papa. Padri aliyehamishiwa Roma alipewa kanisa na lililoitwa Titular Church. Padri huyu alijulikana kama Cardinal-Priest (Kardinali-Padri) na hiyo ikawa aina ya kwanza ya makardinali.
Baadhi ya mashemasi waliohamishiwa Roma walipewa kazi tofauti ikiwemo vituo vya huduma za kijamii vilivyojulikana kama deaconry. Hawa waliitwa Cardinal-Deacon (Kardinali-Shemasi) wakawa ni aina ya pili ya makardinali.
Ofisi ya Papa ilihitaji msaada wa maaskofu hasa wa majimbo madogo jirani na Roma yaliyoitwa “Suburbicarian Diocese”. Kuhitajika Roma kuliwapa maaskofu hawa sifa ya ukardinali, wakajulikana kama Cardinal-Bishop (Kardinali-Askofu) na kuwa aina ya tatu ya makardinali.
Hivyo, aina tatu za makardinali ni Cardinal-Deacon, Cardinal-Priest na Cardinal-Bishop. Sina hakika kama tafsiri yake ni Kardinali-Shemasi, Kardinali-Padri na Kardinali-Askofu.
Mwaka 1150 liliundwa jopo linaloendelea kuitwa College of Cardinals au jopo la makardinali wote. Papa alipenda kuwaita makardinali kwenye vikao vilivyoitwa Consistory hadi leo. Consistory huwa ya makardinali wachache walioko Roma ( ordinary consistory) au ya makardinali wote duniani (extraordinary consistory).
Mwaka 1059 ilipitishwa kwamba Papa mpya atakuwa akichaguliwa na jopo la makardinali kwenye mkutano uliopewa jina Conclave linalotumika hadi leo.
Papa Paul VI aliweka umri chini ya miaka 80 uwe sifa ya Kardinali kuhudhuria Conclave. Papa John Paul I ambaye upapa wake ulidumu kwa siku 33 ndiye wa kwanza kuchaguliwa kwa utaratibu huo Agosti 26, 1978.
Je, mlei aweza kupewa ukardinali? Teodolfo Mertel alipewa ukardinali Machi 15, 1858 akiwa hajapewa hata ushemasi. Wengine humuita “lay-cardinal” yaani “kardinali-mlei” ingawa si sahihi kwani wenye madaraja madogo (minor orders) kama alilokuwa nalo yaani first tonsure yalihesabiwa kama ukleri wakinyoa vipara vidogo na si ulei kama ilivyo sasa.` Hata hivyo utata wake haukudumu kwani kesho yake alipewa daraja la ushemasi na Papa Pius IX.
Mwaka 1917 Cardinal-Deacons walitakiwa wawe mapadri na mwaka 1962 kila kardinali alitakiwa awe askofu. Upadri ukabaki kuwa sifa ya chini (qualification) ya mkatoliki kuchaguliwa kuwa kardinali hadi leo {Rejea: Can. 351(1)}.
Hata hivyo, Papa anaweza kuruhusu padri aliyeteuliwa kuwa Kardinali aendelee na upadri wake bila kupewa uaskofu. Imefanyika hivyo kwa mapadri Avery Dulles, Roberto Tucci na Albert Vanhoye wa shirika moja maarufu kama majesuit na bila kumsahau Padri Yves Congar ambaye ni marehemu.
Mapadri hawa huvaa mavazi ya kiaskofu lakini hawawezi kumpa mtu upadrisho, ushemasi, au uaskofu kwa sababu si maaskofu ingawa ni makardinali (Rejea: Katekism 1576).
Hadi leo aina za makardinali zimeendelea kuwa tatu ingawa wote sasa ni maaskofu isipokuwa kwa ruhusa kama tulivyoona.
Leo hii Cardinal-Bishops wako sita wakipewa Suburbicarian Diocese. Mkuu wa jopo la makardinali au Dean of Cardinals anaongezewa jingine liitwalo Ostia na kufanya majimbo yale kuwa saba. Wanaishi Roma na hufanya kazi kwenye idara (Dicasteries) za kanisa pale Vatican.
Cardinal-Deacons wengi wanaishi Roma pia. Bado hupewa vituo vya ushemasi japo leo vituo hivi huweza kuitwa makanisa (Titular Chuch). Mfano, Kardinali Joseph Levada alimrithi Kardinali Joseph Ratzinger (Papa wa sasa) kuongoza idara ya Doktrina ya imani (CDF). Kituo chake (deaconry au kanisa) kinachoambatana na ukardinali wake ni Santa Maria in Domnica.
Cardinal-Priest (Kardinali-Padri) wengi hawaishi Roma. Mfano ni Polycarp Pengo ambaye kanisa lake huko Roma linaitwa Nostra Signora de La Salette. Yeye ni mjumbe wa idara za Doktrina ya imani (CDF) na Uinjilishaji (CEP). Pia ni mjumbe wa mabaraza mawili yanayosimamia majadiliano na dini nyingine (PCID) na tamaduni mbalimbali (PCC).
Kwa nini Cardinal-Priests wengi hawaishi Roma? Mtaguso wa Trent kwenye kikao (Session) cha 23 ulipitisha hati iliyoitwa Decree Concerning Reform iliyotaka kila aliye mchungaji, lazima akae na watu wake anaowaongoza hata kama ni kardinali. Hivyo Kardinali Pengo anaishi D’Salaam kwa sababu ya jukumu jingine tofauti na ukadinali ambalo ni uaskofu wa jimbo hilo.
Mpangilio wa makardinali kwa hadhi (seniority) kutoka juu kwenda chini ni Cardinal-Bishops, kisha Cardinal-Priests na mwisho ni Cardinal-Deacons. Kwenye sheria za Kanisa (Canon Laws) ukardinali umeelezwa kwenye kanuni ya 349 hadi 359.
Majimbo au makanisa yao kule Roma sasa yanaendeshwa na maaskofu au mapadri wengine ingawa bado yanatolewa kwa makardinali kama ilivyokuwa asili.
Papa anaweza kumtunuku mtu ukardinali kwa siri bila kumuambia yeyote na hata mhusika mwenyewe. Kardinali wa aina hii huitwa Cardinal in pectore au kardinali wa siri. Askofu Ignatius Kung Pin-mei wa Shanghai nchini China alipewa ukardinali wa aina hii Juni 30, 1979 wakati yeye hana habari tena akiwa gerezani akitumikia kifungo kutoka serikali ya kikomunisti ya China iliyokuwa haielewani na kanisa.
Ukardinali wake ulitangazwa wazi Juni 28, 1991 miaka mitatu baada ya kutoka kifungoni. Papa akifariki bila kuwatangaza makardinali hawa, basi ukardinali wao (in pectore) hautambuliki tena labda kama ilikuwa imeandikwa kwenye karatasi (testament). Hivyo Papa ndiye mwenye kujua idadi halisi ya makardinali duniani.
Ukardinali haukutajwa kwenye Katekism ya Kanisa Katoliki wala Biblia. Kwa heshima makardinali huitwa “Princes of the Church” au “Wana watukuka wa Kanisa” . Wanapotambulishwa hutumika neno “Eminence” ambapo kiswahili limetumika neno “Mwadhama”.
Kumtaja Kardinali yawezekana kutumia mtindo wa kilatini mfano Polycarp Kardinali Pengo au wa kiingereza yaani Kardinali Polycarp Pengo.
Suala la Makanisa ya wakatoliki wa Mashariki (Eastern Churches) limefundishwa kwenye hati tatu za Mtaguso mkuu wa Vatican (Vatican II). Ni vizuri kuzirejea sehemu zake ambazo ni Orientalium Ecclesiarum sehemu ya 7-11, Lumen Gentium sehemu ya 23 na Decree on Ecumenism sehemu ya 14-17.
Wakati hili letu la Magharibi (Western Church) linaongozwa kutoka Roma yale ya mashariki yanaendeshwa na wakuu waitwao Patriarch au Patriaka. Sita kati ya makanisa hayo yaliyo 22 ni Melkite Greek, Koptik, Syria, Chaldean, Armenia, Maronite.
Yote hayo yanatambua nafasi ya Papa au askofu wa Roma kama kiongozi wa ukatoliki duniani. Yote hayo na hili letu yana hadhi sawa hakuna linalomzidi mwenzake (Rejea: Orientalium Ecclesiarum sehemu ya 3).
Kardinali Ignace Tappouni alikuwa ni Patriaka wa Antiokia na kiongozi wa Kanisa Katoliki la Syria tangu 1929 hadi 1968. Alipewa ukardinali mwaka 1935 kama Cardinal-Priest. Kwenye kitabu cha Askofu Method Kilaini kiitwacho “Tulivyomfahamu Kardinali Rugambwa”, kardinali huyu au Patriaka anaonekana kwenye picha ya pili ukurasa wa 89 akimpongeza Laurian Rugambwa kuwa mwafrika wa kwanza kupewa ukardinali.
Baada ya Mtaguso (Vatican II) mapatriaka walipewa ngazi ya Cardinal-Bishop lakini wakitambulika kwa majimbo yao wanakoishi bila kupewa majimbo yale “Suburbicarian Diocese” .
Kardinali Stephanos I Sidarouss aliyekuwa Patriaka wa Alexandriakwa Kanisa Katoliki la Koptik alishiriki Conclave zote mbili za mwaka 1978, yaani ile ya Agosti iliyomchagua Papa John Paul I na ile ya Oktoba iliyomchagua Papa John Paul II.
Kardinali Nasrallah Pierre Sfeir, ambaye ni mlebanon, hadi sasa ni Patriaka wa Antiokia kwa Kanisa la Maronite. Hakushiriki Conclave ya mwaka 2005 iliyomchagua Papa Benedict XVI kwani alishavuka umri wa miaka 80. Lakini alionekana akisaidiana (co-celebrate) na Kardinali Joseph Ratzinger ilipowadia liturjia ya Ekaristi kwenye misa ya mazishi ya Papa John Paul II.
Hivyo, kwa sababu mapatriaka hawa wana haki ya kupiga au kupigiwa kura kwenye Conclave, basi haki hiyo inatoa uwezekano wa mmoja wao kuchaguliwa kuwa Papa. Hivyo upo uwezekano wa kumpata Papa kutoka katika haya makanisa ya mashariki.
Je, ukardinali ni kiunganishi cha maaskofu nchini? Heshima ya ukardinali ni kubwa. Lakini tumeona yawezekana kumpata Kardinali ambaye ni padri lakini si askofu. Na zamani ni Cardinal-Bishop tu ndiyo walikuwa maaskofu.
Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania ni Askofu T. Ngalalekumtwa wa jimbo la Iringa. Ndiye anayeongoza baraza hilo linalounganisha maaskofu wote nchini kwa mujibu wa Sheria za Kanisa na kwa mambo wanayokubaliana (Rejea Sheria za kanisa: Can. 447 hadi 459).


Na Fr
Andrew Lupondya

Chapisha Maoni

 
Top